ĐÓMAPµĽş˝

Uvumi wa kwamba Papa Francisko anakusudia kujiuzuri hauna mvuto wala mashiko, jambo la msingi kwa sasa ni afya ya Baba Mtakatifu ili aweze kurejea tena katika maisha na utume wake. Uvumi wa kwamba Papa Francisko anakusudia kujiuzuri hauna mvuto wala mashiko, jambo la msingi kwa sasa ni afya ya Baba Mtakatifu ili aweze kurejea tena katika maisha na utume wake.  (VATICAN MEDIA Divisione Foto)

Kardinali Parolin: Uvumi Kuhusu Kujiuzuru Kwa Papa Francisko Hauna Mvuto Wala Mashiko

Jambo la msingi kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, Baba Mtakatifu anapata matibabu muafaka, ili aweze kusimama tena na hatimaye, kurejea mjini Vatican kuendelea na utume wake. Haya ni majibu yaliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin katika mahojiano maalum na Gazeti la “Corriere della Sera." Tangu Papa alazwe, tarehe 14 Februari 2025, kumekuwepo na uvumi, uzushi na habari za kughusi kuhusu afya ya Baba Mtakatifu na kwamba, ameonesha kutaka kung'atuka.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema, kuna uvumi usio na maana, mvuto wala mashiko kuhusu kujiuzuru kwa Baba Mtakatifu Francisko baada ya kuugua na hatimaye kulazwa kwenye Hospitali ya Chuo Kikuu cha Agostino Gemelli, iliyoko mjini Roma. Jambo la msingi kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, Baba Mtakatifu anapata matibabu muafaka, ili aweze kusimama tena na hatimaye, kurejea mjini Vatican kuendelea na utume wake. Haya ni majibu yaliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin katika mahojiano maalum na Gazeti la “Corriere della Sera” linalochapishwa kila siku nchini Italia. Tangu Baba Mtakatifu Francisko alazwe, tarehe 14 Februari 2025, kumekuwepo na uvumi, uzushi na habari za kughusi kuhusu afya ya Baba Mtakatifu na kwamba, ameonesha dalili za kutaka kung’atuka kutoka madarakani.

Kardinali Pietro Parolin: Uvumi wa Papa Kujiuzuru hauna mvuto wala mashiko
Kardinali Pietro Parolin: Uvumi wa Papa Kujiuzuru hauna mvuto wala mashiko   (Vatican Media)

Huu ni uvumi unaoihusisha Vatican na kwamba, Kardinali Parolin binafsi hajasikia uvumi huu, wala mipango ya Baba Mtakatifu Francisko kutaka kung’atuka. Katika hali na mazingira kama haya, si ajabu kuona watu wakiandika habari za kughushi zisizo kuwa na mvuto wala mashiko na kwamba, hii si mara ya kwanza uzushi kama huu kutolewa na watu wenye nia mbaya. Kardinali Parolin, hivi karibuni amerejea kutoka Burkina Faso na alipozungumza na Baba Mtakatifu, akamwambia kwamba, yuko tayari kumtembelea hospitalini ikiwa kama ataona inafaa, lakini hadi sasa hakuna sababu msingi za kumtembelea Baba Mtakatifu Francisko hospitalini, kwani anatakiwa kuwa na muda wa mapumziko. Habari kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Agostino Gemelli zinaendelea kutia moyo kwamba, hali ya afya ya Baba Mtakatifu inaendelea kuimarika kila kukicha!

Jambo la msingi ni kuona afya ya Papa inaendelea kuimarika
Jambo la msingi ni kuona afya ya Papa inaendelea kuimarika   (VATICAN MEDIA Divisione Foto)

Wakati huo huo, Kardinali Víctor Manuel Dias Fernández, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafunfundisho Tanzu ya Kanisa, katika mahojiano maalum na Gazeti la La Naciòn” linalochapishwa nchini Argentina anasema, haina maana kwa baadhi ya makundi yanayotaka kumshinikiza Baba Mtakatifu Francisko kung’atuka kutoka madarakani. Hii ni kampeni ambayo kwa miaka kadhaa sasa wanaifanya. Lakini ikumbukwe kwamba, kung’atuka kwa halali kwa Baba Mtakatifu Francisko kutoka madarakani lazima iwe ni kwa ridhaa yake mwenyewe na wala si vinginevyo. Kumbe, hapa hakuna habari mpya, yote ni ya zamani! Kardinali Víctor Manuel Dias Fernández anakaza kusema, jambo la muhimu kwake ni kuona kwamba, afya ya Baba Mtakatifu Francisko inaendelea kuimarika zaidi.

Uvumi Usio na Mashiko

 

22 Februari 2025, 14:30