Papa na Uwakilishi wa Kibudha kutoka Mongolia:Tujenge mshikamano kati ya watu na nyumba ya pamoja!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Papa Francisko, Jumatatu tarehe 13 Januari 2025, alikutana na Uwakilisi wa Wabudha kutoka nchini Mongolia, ambapo katika hotuba yake alikuwa na furaha kubwa kuwasalimu wote hasa kuanzia na D. Javzandorj, Abate wa Monasteri ya Gandantegchinlen huko Ulaanbaatar, pamoja na Mwadhama Kardinali Giorgio Marengo, Mwakilishi wa Kitume wa Ulaanbaatar. Ziara yao ya kwanza mjini Vatican alisema Papa ilikuwa na umuhimu wa kipekee kwani iliakisi uhusiano wa kirafiki na wa kudumu kati ya Vatican na watu mashuhuri wa Mongolia, urafiki ambao alipata fursa ya kuwa nao wakati wa ziara yake ya Kitume kwa nchi yao mwaka 2023. Jambo kuu la ziara hiyo lilikuwa ni katika Mkutano wa kidini ambamo walitafakari juu ya hamu kubwa ya kiroho ya wanaume na wanawake wote, ambao tunaweza kuwafananisha na kundi kubwa la akina kaka na dada wanaosafiri maishani wakiwa wameinuliwa kwenda mbinguni. Kwa hivyo Papa amewakaribisha wote “kama ndugu wote katika jina la jitihada yetu ya pamoja ya kidini” (Hotuba kwa Mkutano wa Kiekumene na Kidini, Ulaanbaatar, 3 Septemba 2023).
Nchi yao imepitia upya wa kidini tangu miaka ya 1990, ambayo hata hivyo ameipongeza kujitolea na michango yao. Kwa kufufua mazoea ya kiutamaduni ya kiroho na kuyajumuisha katika maendeleo ya taifa, Mongolia imerudisha urithi wake tajiri wa kidini huku ikionesha kujitolea kwake kwa mabadiliko ya kidemokrasia yenye mafanikio. Zaidi ya hayo, kujitolea kwao kwa uhuru wa kidini na mazungumzo kati ya madhehebu mbalimbali ya kidini kumekuza nafasi ya kuheshimiana kwa mapokeo yote na kukuza jamii iliyotajirishwa, si tu kwa ustawi wa mali, bali pia maadili muhimu kwa mshikamano wa kidugu. Papa Francisko aidha alisisitiza kuwa katika kukuza maadili haya, dini zina jukumu muhimu katika kujenga jamii yenye haki na mshikamano. Ziara yao wenyewe inafanyika kuelekea mwanzoni mwa Mwaka huu wa Jubilei. Katika mapokeo ya Kikristo, huu ni wakati wa hija, upatanisho na matumaini. Katika wakati uliogubikwa na majanga ya asili na migogoro ya kibinadamu, Mwaka huu Mtakatifu unatuita kwenye lengo la pamoja la kujenga ulimwengu wa amani zaidi ambao unakuza utangamano kati ya watu na nyumba yetu ya pamoja.
“Shauku ya ulimwengu kwa ajili ya amani inatupatia changamoto sisi sote kuchukua hatua madhubuti. Kwa namna fulani, kama viongozi wa kidini waliokita mizizi katika mafundisho yetu husika, tunabeba jukumu la kuhamasisha ubinadamu kuachana na vurugu na kukumbatia utamaduni wa amani. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba muda wao jijini Roma utakuwa wa kufurahisha na kutajirika, na kwamba mkutano wao na Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini utatumika kama fursa ya kuimarisha ushirikiano katika kukuza jamii inayosimikwa kwenye mazungumzo, udugu, uhuru wa kidini, haki kijamii na maelewano. Papa aliwahimiza wavumilie katika kukuza kanuni hizo na katika kuimarisha uhusiano na Kanisa Katoliki nchini Mongolia, kwa ajili ya amani na ustawi wa wote. Kwao na wale wote wanaowawakilisha katika monasteri za Wabuddha za Mongolia, Papa Francisko aliwatakia heri zake na maombi. Na wabaki thabiti katika kujitolea kwao, wenye bidii katika huruma na wenye furaha katika tumaini, alihitimisha.