Rais Volodymyr Zelensky akutana na Papa Leo XIV Castel Gandolfo
Na Sarah Pelaji, -Vatican.
Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky amekutana na Papa Leo XIV katika kikao chao cha faragha kilichofanyika Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo mnamo Jumatano tarehe 9 Julai 2025, huku mazungumzo yao yalijikita katika vita vinavyoendelea nchini Ukraine na umuhimu wa kutafuta amani kwa njia ya mazungumzo. Mazungumzo hayo yalihusu juhudi za kumaliza vita na hivyo kutafuta suluhisho la haki na la kudumu kwa vita vya Ukraine. Papa alieleza masikitiko yake kwa waathirika wa vita na kuwahakikishia wananchi wa Ukraine sala na ukaribu wake wa daima. Aidha, Baba Mtakatifu Leo XIV alihimiza juhudi za kuwaachilia wafungwa na kuwarejesha watoto waliotenganishwa na familia zao. Alirudia tena kutoa mwaliko wa Vatican kuwa tayari kuwapokea wawakilishi wa Ukraine na Urusi kwa ajili ya mazungumzo ya amani.
Baada ya mkutano huo, Rais Zelensky alizungumza kwa kifupi na waandishi wa habari kwa lugha ya Kiingereza akieleza jinsi alivyofurahi kupata nafasi adhimu ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Leo XIV, huku akiishukuru Vatican kwa msaada wake, hasa kuhusu suala la watoto wa Ukraine waliotekwa na kupelekwa Urusi wakati wa vita. “Hili ni jambo muhimu sana ambalo tumelizungumzia,” alisisitiza Zelensky huku akieleza umuhimu wa kuwarudisha watoto hao kwa ndugu zao nchini Ukraine. Mintarafu dhamira ya Ukraine kutafuta amani Rais Zelensky aleleza: “Bila shaka tunataka amani, tunataka vita kumalizika. Tunategemea sana msaada wa Vatican na wakati huu tunamhitaji sana Baba Mtakatifu Leo XIV katika kutoa mahali pa kufanyika mkutano wa viongozi wa juu ili kumaliza vita hivi.”