Maaskofu wapya waliowekwa wakfu walishiriki kozi ya malezi mjini Vatican!
Na Angella Rwezaula - Vatican
Kwa ujumla ni Maaskofu 267 walioteuliwa hivi karibuni kutoka mabara 5(takriban wote waliowekwa wakfu katika mwaka uliopita), ambao wamekusanyika mjini Vatican siku hizi ili kushiriki kozi hiyo kuanzia tarehe 15 hadi 22 Septemba 2024 katika Mafunzo Maalum yaliyotolewa na Mabaraza mbalimbali ya kipapa mjini Vatican. Hayo yalielezwa na Shirika la Habari za Kimisionari Fides, ambalo pia ni mojawapo ndani ya wahusika wakuu wa Maandalizi ya tukio la Kozi hizi za maaskofu wapya. Kwa njia hiyo “Ratiba ya mwezi Septemba ambayo sasa imekuwa ya kawaida na utamaduni katika kupanga shughuli za Curia Romana, na ambayo mwaka huu 2024 imechukua dhana mpya kwa sababu “kwa mara ya kwanza, sehemu nzuri ya vikao vya kazi imeshirikishwa na uzoefu wa pamoja katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana Mjini Roma na Maaskofu wote wa pande mbili za Kanda walioshiriki katika kozi iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Uinjilishaji (Sehemu ya Uinjilishaji wa kwanza na Makanisa mapya hasa) na wale wanaoshiriki katika mafunzo sawa yaliyoandaliwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu.
Kwa undani zaidi Maaskofu walioshiriki Kozi ya Baraza la Kipapa la Uinjilishaji ni 114, huku washiriki wa Kozi hiyo iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa la Maaskofu Maaskofu ni 153. Miongoni mwa Maaskofu hao wamo pia Maaskofu 25 wa Ibada ya Mashariki(ambao ni wa kanda ya Mashariki) yenye marejeo ya Makanisa ya Mashariki) na Maaskofu 5 waliowekwa wakfu hivi karibuni wakiwa na majukumu katika Ofisi za Curia Romana. Vikao vya kazi vya pamoja vilivyoandaliwa katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Urbaniana, vilifunguliwa Jumanne tarehe 17 Septemba 2024 na ripoti iliyowasilishwa na Sekretarieti ya Vatican kuhusu: “hatua ya Vatican katika ulimwengu wa utandawazi”, na kuhitimishwa tarehe 18 Septemba 2024 kwa hotuba ya Kardinali Kevin Joseph Farrell, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Walei Familia na Maisha akijikita na mada: “Utume wa Walei.” Katika siku nyingine za Kozi, makundi mawili ya Maaskofu walisikiliza ripoti na kushiriki katika mijadala iliyojikita katika masuala maalum katika maeneo mawili tofauti: Kozi iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa la Uinjilishaji, kwa mada ya: “Kuishi Utume wa Maaskofu katika Kanisa la Kisinodi” iliyofanyika katika Chuo cha Kipapa cha Mtakatifu Pietro, wakati kozi iliyoandaliwa na Baraza la Maaskofu ilifanyika katika Chuo cha Kipapa cha Mtakatifu Paulo.
Kazi ya kozi ya mafunzo kwa Maaskofu wapya iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Uinjilishaji (Sehemu ya Uinjilishaji wa kwanza na Makanisa mapya) ilianza asubuhi ya Jumatatu tarehe 16 Septemba 2024 kwa hotuba ya Kardinali Luis Antonio Tagle, Mwenyekiti Mwenza wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji na Askofu Mkuu Fortunatus Nwachukwu (Katibu Mkuu wa Baraza hilo la Kimissionari) na Askofu Mkuu Emilio Nappa (Katibu Msaidizi wa Kitengo cha Kimisionari na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya). Makundi mawili ya Maaskofu wapya walikutana na Baba Mtakatifu Francisko ambapo kundi la kwanza lililoandaliwa na Baraza la Kipapa Maaskofu ilikuwa ni Alhamisi tarehe 19 Septemba 2024, huku kundi la pili ambalo lilishiriki kozi iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa la Uinjilishaji, lilikutana na Baba Mtakatifu, Jumamosi, tarehe 21 Septemba 2024 ikiwa ni kilele cha Juma la kazi. kwa njia hiyo kundi lilipata uzoefu kama ishara na tafakari ya ushirika unaokumbatia na kuunganisha Kanisa la Ulimwengu na kama wakati wa ushirikiano, ujuzi wa pamoja, ujenzi unaowezekana wa vifungo kati ya Makanisa mbalimbali mahalia.
Desturi ya kozi ya iliyotengwa kwa ajili ya Maaskofu wapya waliowekwa wakfu hivi karibuni katika madaraja ya kikanisa waliokabidhiwa uangalizi wa Mabaraza ya kimisionari ilianzishwa mwaka 1994, kwa lengo la kuwapa Maaskofu wote wapya kipindi cha muda mwanzoni mwa kazi yao ili kuzingatia athari nyingi za zoezi la huduma ya Maaskofu, kusikiliza mijadala, kupata habari na kuishi Roma na siku zilizoadhimishwa na mazungumzo na sala, ambazo zilishirikishwa na ndugu katika uaskofu kutoka sehemu zote za ulimwengu. Katika kipindi hiki cha kujifunza na kujitajirisha kiroho, Maaskofu wapya walipewa nafasi ya kukutana pamoja na Papa Francisko, wakaadhimisha Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro na makanisa mengine jijini Roma, na kushirikiana na watu wakuu kutoka katika Mabaraza ya Kipapa, wakiwemo wakuu wa mabaraza mbalimbali ya Kipapa na wawakilishi kutoka Sekretarieti ya Vatican. Zaidi ya hayo, washiriki walifanya kazi katika vikundi vidogo vinavyotegemeana na lugha ili kuhamasisha mazungumzo ya kina. Waandaaji walieleza kwamba hizi ni “siku nzito zilizojaa nyakati za malezi na umoja zinazowapa Maaskofu wapya uzoefu wa kina kwa umoja wa Maaskofu, ambao unakuza umoja wa upendo na ufanisi na Mrithi wa Petro.” Mabaraza ya Kipapa yaliyopewa jukumu la kumsaidia Baba Mtakatifu katika mchakato mgumu wa kuwateua Maaskofu wameeleza kuridhishwa kwao na matokeo yenye matunda ya kozi hiyo.
Akitafakari juu ya umuhimu wa tukio hilo, kwa waandishi wa habari mjini Vatican, Askofu S?awomir Szkredka, Askofu Msaidizi wa Los Angeles, alishiriki, “Kozi hii ya malezi ina umuhimu mkubwa kwa sababu tatu. Kwanza, inatoa uzoefu wa umoja, kukutana na Baba Mtakatifu,ambaye ni Mtume Petro wa wakati wetu na kushuhudia hali ya jumla ya Kanisa pamoja na ndugu zetu kutoka duniani kote. Pili, linatoa zawadi ya kukutana na maaskofu wenzetu kutoka makanisa mbalimbali, kutuwezesha kubadilishana uzoefu, kujenga mahusiano na kuomba pamoja. Hatimaye, tunashirikiana na wawakilishi kutoka Mabaraza ya Kipapa ambao wanawasilisha maono ya Papa Francisko, wakituruhusu kutafakari jinsi gani tunaweza kutumika katika Makanisa yetu mahalia katika maeneo mbalimbali.”
Katika ya Maaskofu hao wapya kutoka Ulimwenguni kote, kuna Maaskofu wapya kutoka nchini Tanzania ambao ni: Askofu Vincent Cosmas Mwagala wa Jimbo Katoliki la Mafinga, Askofu Thomas, John Kiangio wa Jimbo Katoliki la Tanga, Askofu Wilibroad Henry Kibozi, Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dodoma, Askofu Eusebio Samwel Kyando wa Jimbo Katoliki la Njombe, Askofu Godfrey Jackson Mwasekaga, Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Mbeya na hatimaye Askofu Jovitus Francis Mwijage wa Jimbo Katoliki la Bukoba.