杏MAP导航

Tafuta

2025.05.19 Papa na Patriaki Bartolomeo I, wa Costantinopoli 2025.05.19 Papa na Patriaki Bartolomeo I, wa Costantinopoli  (@Vatican Media)

Papa Leo XIV akutana na Patriaki umuhimu wa kuimarisha majadiliano ya kitaalimungu!

Jumatatu tarehe 19 Mei Baba Mtakatifu Leo XIV alikutana na Patriaki wa kiekumene katika Jumba la Kitume na katika mazungumzo yao wamesisitiza umuhimu wa kukuza na kuimarisha majadiliano ya kitaalimungu kati ya Kanisa la Kiorthodox na Katoliki na kujitolea kwa ajili ya amani na mazingira.Alasiri Patriaki huyo alikwenda kusali mbele ya kaburi ya Papa Francisko katika Kanisa kuu la Mtakatifu Maria Mkuu.

Na Angella Rwezaula – Vatican.


Papa Leo XIV alimhakikishia Patriaki wa Kiekumeni Bartholomew I shauku yake ya dhati ya kusafiri hadi Uturuki, ndani ya mwaka huu na tarehe itakayopangwa, kuadhimisha pamoja na Patriaki kumbu kumbu ya miaka 1700 tangu kufanyika kwa Mtaguso wa kwanza wa Kiekumene wa Nicea." Hivi ndivyo Patriaki wa Kiekumene alitangaza katika taarifa yake iliyotolewa kwenye ukurasa wao wa upatriaki kuhusiana na mkutano ambao Patriaki huyo alikuwa nao Jumatatu tarehe 19 Mei 2025 mjini Vatican na Papa Leo XIV.

Mazungumzo ya Patriaki wa kiekumene na Papa Leo
Mazungumzo ya Patriaki wa kiekumene na Papa Leo   (@Vatican Media)

Katika  taarifa hiyo aidha inabainisha kuwa wakati wa mkutano huo mzuri, Patriaki Bartholomew binafsi alimpongeza Papa mpya Leo XIV  kwa kuchaguliwa kwake na katika mazungumzo hayo alisisitiza, pamoja na mambo mengine, umuhimu wa kuendelea kukuza na kuimarisha mazungumzo ya kitaalimungu kati ya Makanisa mawili, yaani ya Kiorthodox na Kanisa Katoliki la Roma, pamoja na ushirikiano wao katika masuala ya maslahi ya kijamii, kama vile kurejesha na kudumisha amani duniani, kusaidia watu wanaoteseka na mazingira. Patriaki huyo pia alitaja uhusiano na ushirikiano wa kidugu aliokuwa nao na hayati Papa Francisko, ambaye alikutana naye zaidi ya mara kumi.

Mkutano na Patriaki wa kiekumene
Mkutano na Patriaki wa kiekumene   (@Vatican Media)

Baba Mtakatifu Leo XIV hata hivyo alitoa shukrani zake kwa Patriaki huyo kwa uwepo wake katika Misa ya ufunguzi  wa huduma yake ya Mfuasi wa Mtume Petro na pia kusisitiza umuhimu wa kukuza mazungumzo na ushirikiano wa kiekumene. Kuhusu hija ya Nicea, Upatriaki wa kiekumene ulikumbusha kwamba Patriaki Bartholomw I pia alikuwa amemwalika Hayati Papa Francisko kwa kusudi hilo na kwa hivyo akafanya kwa upya mwaliko wake kwa mrithi wake Papa Leo XIV.

Wakati wa kubadilishana zawadi
Wakati wa kubadilishana zawadi   (@Vatican Media)

Wakati wa kubadilishana zawadi, Patriaki wa Kiekumene alimpatia Papa Leo XIV sanamu ya Bikira Maria Hodegetria, iliyochorwa kwenye Mlima Athos, uvumba wa miski uliotayarishwa na watawa wa Athonite na vitabu vyake. Papa alimpatia Patriaki Bartholomew uwakilishi wa kisanii wa ubatizo wa Bwana. Baadaye, katika Ukumbi wa Clementine mjini Vatican, Papa aliwakaribisha na kuzungumza na wawakilishi wa Makanisa na dini nyingine, waliohudhuria Dominika tarehe 18 Mei 2025 katika ibada ya Misa ya kuanza kwake huduma ya Mfuasi wa Petro ambapo aliwasalimia mjumbe mmoja moja.

Kutembelea kaburi la Papa Francisko

Mapema alasiri, Patriaki na wasaidizi wake walitembelea Ubalozi wa Jamhuri ya Uturuki. Kutoka hapo, Patriaki wa Kiekumene alikwenda moja kwa moja kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Maria Mkuu, ambako alisali na kuweka maua meupe kwenye kaburi la Hayati Baba Mtakatifu Francisko. Patriaki baada ya hapo alitembelea kwa hisia Taasisi ya Kipapa ya Mafunzo ya Mashariki, ambako alisomea katika miaka ya 1963-1966, akibobea katika Sheria za Kanisa.

Patriaki wa Costantinopoli alitembelea kaburi la rafiki yake Papa Francisko

Papa Leo XIV na Patriaki wa kiekumene
19 Mei 2025, 21:52