Papa Francisko atuma telegramu nchini Korea kufuatia na moto mkali
Vatican News
Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa tarehe 28 Machi 2025 ametuma telegramu yake iliyotowa saini na Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican kwa Mamlaka ya kikanisa na kiraia, nchini Korea Kusini kufuatia na moto mkubwa uliozuka msituni ambapo hata rais wa Nchi hiyo Jumatano tarehe 26 Machi, alitangaza kuwa “moto huo ulileta uharibifu mkubwa usio wa kawaida na kuzidi makadirio yote yaliyofanywa hapo awali.”
Katika telegramu ya Baba Mtakatifu Francisko inaeleza kuwa ameguswa sana na tishio la maisha na uharibifu unaosababishwa na moto wa msituni ambao umesambaa hata sehemu mbali mbali za Korea. Kwa njia hiyo Baba Mtakatifu anaziweka “roho za marehemu katika Huruma wa upendo wa mwenyezi Mungu na anawapa pole wale wote wanaoomboleza kwa ajili ya wapendwa wao.” Baba Mtakatifu aidha anasali kwa ajili ya majeruhi na kwa ajili ya juhudi za misaada ya wazima moto na watu wengine wa dharura. Na juu ya wote anawaombea Baraka za faraja ya uponyaji na nguvu kutoka kwa Mungu.”
Vyombo vya ndani vya mawasiliano vinaeleza kuwa Zaidi ya ekari elfu 43 za ardhi zimeteketea, majengo zaidi ya mia mbili yameharibiwa ikiwemo hekalu la kale yenye umri wa miaka 1,300 pamoja na viwanda na magari mengi. Maeneo yaliyoathirika zaidi ni miji ya Andong, Uiseong, Sancheong na Ulsan. Zaidi ya wazima moto elfu tisa, helikopta mia moja na thelathini na mamia ya magari wanaendelea kupambana na moto huo licha ya hali ya hewa kavu na upepo mkali unaozuia juhudi zao. Serikali imesema bado moto huo haujadhibitiwa kikamilifu.