Papa amekutana na vijana wa Kituruki waliokumbwa na tetemeko la ardhi
Na Angella Rwezaula, - Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi tarehe 3 Agosti 2023 aliporudi Ubalozi wa Vatican nchini Ureno baada ya asubuhi ya siku ya pili akiwa huko Lisbon ambapo alikuwa ametumia muda wake kwanza ibada ya misa, kukutana na wanafunzi vijana wa Chuo Kikuu Katoliki na wanafunzi wa Scholas Occurrentes, alikutana pia na kikundi cha vijana wapatao 40 wa kutoka madhehebu mbalimbali ya Kikristo na asili tofauti, ambao ni mahujaji kutoka Uturuki, wakishiriki WYD na nchi ambayo iliyokumbwa na tetemeko la ardhi mwanzoni mwa mwezi Februari mwaka huu, wakiambatana na Mkuu wa Vikaria ya Kitume ya Anatolia nchini humo.
Hayo yametangazwa na Ofisi ya Vyombo vya Habari Vatican, ikieleza kwamba vijana hao walimshukuru Baba Mtakatifu kwa msaada walioupata baada ya tetemeko la ardhi. Papa Fransisko alionesha ukaribu wake na mateso yanayowapata wale waliopatwa na uharibifu uliosababishwa na tetemeko la ardhi, akitambua “ujasiri wao na changamoto ya kujenga upya, hata katika maisha.” Kwa hiyo katika mkutano huo uliochukua takribani nusu saa na kuhitimishwa kwa sala ya Baba Yetu, pia ilisherehekewa siku ya kuzaliwa ya msichana mmoja wa Kituruki, ambaye anatimiza miaka 23 tarehe 3 Agosti 2023.