杏MAP导航

Tafuta

2025.08.16 Tanzania Askofu Jovitus F. Mwijage,aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kanisa la Kigango cha Ihunga na kuzindua Kanisa la Kigango cha Mtakatifu Petro Mtume Mabira,Bukoba. 2025.08.16 Tanzania Askofu Jovitus F. Mwijage,aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kanisa la Kigango cha Ihunga na kuzindua Kanisa la Kigango cha Mtakatifu Petro Mtume Mabira,Bukoba. 

Tanzania,Ask.Mwijage: kila familia inayo wajibu wa kulinda Imani Katoliki bila kuyumbishwa!

Katika Ziara ya kichungaji katika Parokia ya Rukindo,Jimbo Katoliki Bukoba,Askofu Mwijage katika mahubiri alisisitiza wajibu wa familia kulinda imani katoliki na daima kutoyumbishwa na madhehebu yanayochipuka.Aliomba waamini kulinda watoto ambao ni hazina ya Kanisa.Alisihi waamini kuombea haki na Amani nchini Tanzania wakati nchi inaelekea uchaguzi mkuu,"kwani bila haki hakuna amani."Na alitoakipaimara kwa watoto 2511 wa Parokia hiyo.

Na Patrick  P. Tibanga-Radio Mbiu – Kagera.

Wazazi na walezi wametakiwa kutunza uzao, kuwafundisha watoto wao sala na Imani na kuwaandaa watoto wao katika kuitetea Imani na kuliombea amani taifa la Tanzania.  Rai hiyo imetolewa  tarehe 10 Agosti 2025 na Mhashamu Jovitus Mwijage, Askofu Jimbo Katoliki Bukoba, Tanzania wakati wa homilia yake, kwa waamini wa Kigango cha Mtakatifu Petro Mtume- Mabira, Parokia ya Rukindo,  Jimbo Katoliki Bukoba, alipokuwa katika ziara yake ya kichungaji katika Parokia hiyo.

Askofu Mwijage wa Jimbo la Bukoba Tanzania
Askofu Mwijage wa Jimbo la Bukoba Tanzania

Askofu Mwijage alisema kuwa, kila familia inayo wajibu wa kulinda Imani Katoliki na kamwe wasikubali kudanganyika na madhehebu yanayo chipukia, na kuwasihi wazazi kulinda Kanisa lao na vizazi vijavyo kwa gharama yoyote kwa kuwa na Imani thabiti na kuilinda kupitia matendo mema. “Sehemu zote nilipokwenda katika mataifa ya magharibi ninakuta hakuna silaha ya kulinda Kanisa ambalo ni watoto, wamejenga makanisa mazuri sana, kitu walichokosea walikataa uzao, hawakuwa na majeshi ya kulinda Kanisa, na Makanisa sasa hivi yananunuliwa na wahamiaji kutoka nchi za mashariki ya kati, na hilo ni tatizo kubwa linalokumba makanisa ya Ulaya na Amerika, kwa hiyo ninawaomba wakina baba na mama,  familia tilieni maanani hilo kutunza makanisa, baada ya muda mchache Mungu atatuita kama hakuna majeshi ya watoto ya kulinda na kutunza makanisa, itakuwa kazi bure.” Alisema Askofu Mwijage katika mahubiri yake. Askofu Mwijage alidha aliwataka waamini kuanzisha vyama vya kitume na kuwahimiza watoto kushiriki katika vyama hivyo huku akisisitiza watoto kuwa “ni hazina bora ya Kanisa, pamoja na kutenga muda wa kuabudu Ekaristi Takatifu, kupokea sakramenti ya kitubio na kupeleka mahangaiko yao kwa Yesu wa Ekaristi kila wanapopata nafasi.”

Askofu Mwijage wakati wa ziara yake ya kichungaji,Parokia ya Rukindo,Bukoba
Askofu Mwijage wakati wa ziara yake ya kichungaji,Parokia ya Rukindo,Bukoba

Kuhusu uchaguzi mkuu unaotarajiwa nchini Tanzania hivi karibuni, Askofu Mwijage aliwataka waamini “kuombea haki na Amani nchi Tanzania nakuwasihi viongozi wa Serikali kuhubiri haki na Amani, ili kutenda haki kwa wananchi wake ndio Amani itapatikani” na kuongeza kuwa “ taifa haliwezi kuwa na Amani bila haki kutendeka kwa wananchi wake.”

"Tuombe viongozi wetu, waweze kufahamu watu wanalia hakuna haki, wanaombea haki na amani, wawe tayari kutunza haki ndipo amani itapatikana, neno haki hawataki kulisikia, sisitiza kwanza pawepo haki ndipo amani itapatikana, wengi wanapotosha kwa kusema amani bila ya haki, wengi linawasumbua hawataki kusikia neno haki, sisitiza kwanza pawepo haki ndipo Amani itafuata," alisisitiza Askofu Mwijage katika homilia yake.

Askofu Mwijage wakati wa zira ya kichungaji Parokia ya Rukindo alifanya uzinduzi wa kanisa la Kiganogo cha Mtatakatifu Petro mtume -mabira
Askofu Mwijage wakati wa zira ya kichungaji Parokia ya Rukindo alifanya uzinduzi wa kanisa la Kiganogo cha Mtatakatifu Petro mtume -mabira

Katika ziara hiyo Askofu Mwijage alifanikiwa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kanisa la Kigango cha Ihunga na kuzindua Kanisa la Kigango cha Mtakatifu Petro Mtume Mabira, kisha alihitimisha ziara yake kwa kutoa Sakramenti ya Kipaimara kwa waimarishwa 2511 wa Parokia hiyo.

Askofu Mwijage  katika Uzinduzi wa ujenzi wa kigango wakati wa ziara yake ya kichungaji Parokia ya Rukindo
Askofu Mwijage katika Uzinduzi wa ujenzi wa kigango wakati wa ziara yake ya kichungaji Parokia ya Rukindo

 

16 Agosti 2025, 09:31